CCM Tanzania
CCM Tanzania

CCM Tanzania

@ccmtanzania

Siri zaidi Mtanzania aliyefia Russia
Muktasari:
Siku nne baada ya familia ya Nemes Tarimo (33), Mtanzania aliyefariki dunia vitani Russia kuitaka Serikali kueleza undani wa kifo hicho, Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Dk Stergomena Tax jana alijitokeza na kueleza kisa na mkasa hadi mauti yakamkuta.
Dar es Salaam. Siku nne baada ya familia ya Nemes Tarimo (33), Mtanzania aliyefariki dunia vitani Russia kuitaka Serikali kueleza undani wa kifo hicho, Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Dk Stergomena Tax jana alijitokeza na kueleza kisa na mkasa hadi mauti yakamkuta.
Waziri Tax akizungumza na vyombo vya habari jijini Dar es Salaam, alisema Tarimo kabla ya kufikwa na mauti, alikuwa vitani baada ya kuwa amejiunga na kikundi cha kijeshi cha Russia, Wagner ikiwa ni ahadi ya kujinasua kifungoni.

Alisema tayari mwili wake umesafirishwa jana kutoka Russia kuja Tanzania kwa ajili ya taratibu za mazishi yatakayofanywa na familia yake na kuwa Serikali inaendelea kuwasiliana kwa karibu na Serikali ya Russia.
Januari 20, akizungumza na Mwananchi nyumbani kwao, dada wa marehemu, Salome Kisale alisema familia inaiomba Serikali kutoa tamko ili kujua kijana wao amekufa kwa sababu gani na kama alikuwa hasomi, yale mambo yaliyokuwa yakiandikwa kwenye mitandao yana ukweli gani.

“Tunaomba Serikali itusaidie kutoa tamko kuwa kijana wetu ni kweli amekufa na chanzo kinachosemekana kina ukweli gani ili tuwe tunaelewa, hivi sasa tunachanganyikiwa, taarifa ni nyingi sana,” alisema Kisale.

“Sisi tunafahamu mdogo wetu alienda Russia mwaka 2016 kwa ajili ya kusoma, lakini baada ya kutangazwa kwa kifo chake ndipo tunapoona kuwa amefariki kama mwanajeshi.”

Ufafanuzi wa waziri

Akizungumzia hilo, Dk Tax alikiri kuwa Tarimo alikwenda Russia na kujiunga na Chuo Kikuu cha Moscow Technological University (MIREA) mwaka 2020 kwa masomo ya shahada ya uzamili katika fani ya Biashara na Uchakataji wa Taarifa (Business Informatics).

Alisema taarifa walizonazo, Tarimo aliuawa Oktoba 24, 2022 na alikuwa amejiunga na kikundi cha kijeshi kwa ajili ya kuisaidia Russia kwenye vita kati yake na Ukraine iliyoanza Februari, 2022.
Alisema Machi 2022, Mtanzania huyo alihukumiwa kifungo cha miaka saba jela kwa mujibu wa Sheria za Russia kwa vitendo vya uhalifu ambavyo hakuvitaja.

Waziri alisema wizara yake imepokea taarifa kutoka Serikali ya Russia kwamba akiwa gerezani, Tarimo alipewa nafasi ya kujiunga na kikundi hicho cha kijeshi cha Russia kiitwacho Wagner, kwa ahadi ya kulipwa fedha na kuachiwa huru baada ya kumaliza muda wa kutumika kwenye vita hivyo.

Alisema baada ya mazungumzo hayo, Tarimo alikubali kujiunga na kikundi hicho na hatimaye alielekea vitani nchini Ukraine hadi alipofikwa na umauti Oktoba 24, 2023.

Hata hivyo, Waziri Tax alisema ni kosa kwa Mtanzania kujiunga na jeshi lolote awapo nje ya nchi.

“Ikumbukwe kwamba, kwa mujibu wa sheria zetu, Mtanzania yeyote haruhusiwi kujiunga na jeshi la nchi yoyote isipokuwa la Tanzania tu. Hivyo, nitoe rai kwa Watanzania wote kuhakikisha wanazingatia sheria za nchi yetu, kanuni na taratibu zilizopo.

“Napenda kuuhakikishia umma na diaspora wa Kitanzania, wakiwamo wanafunzi walioko masomoni nchini Russia kuwa, Serikali kupitia Ubalozi wake uliopo Russia itaendelea kuwapatia ushirikiano na kuhakikisha Watanzania hao wako salama wakati wote,” alisema Dk Tax.

Waziri Tax alisema Serikali itahakikisha mwili wa Mtanzania huyo unarejeshwa nchini kwa ajili ya kuzikwa na familia yake na kuwa tayari mwili huo ulishaondoka Russia jana asubuhi kuja nchini.

“Wizara inaendelea kuwasiliana na Serikali ya Russia kuhakikisha mwili wa marehemu Tarimo unarejeshwa nchini na kukabidhiwa kwa familia husika ili utaratibu wa mazishi ufanyike kwa kuzingatia mila na desturi za Kitanzania,” alisema.

Alisema Serikali inatoa pole kwa familia ya marehemu, ndugu na jamaa na Watanzania kwa ujumla kwa msiba huo.

Lakini aliwataka Watanzania kuwa mabalozi wazuri wa kulinda taswira ya nchi wawapo ugenini.

Kwa mujibu wa gazeti la The Moscow Times la Russia, mapema Januari mwaka huu, wafungwa wa kwanza walioandikishwa na kikundi cha kijeshi cha Wagner kutoka jela za nchi hiyo, walimaliza kazi yao ya miezi sita nchini Ukraine na kupokea msamaha walioahidiwa kutoka kwa Serikali ya Russia.

Ripoti za vyombo vya habari zilimnukuu mwanzilishi wa Wagner, Yevgeny Prigozhin akisema:

“Walimaliza mkataba wao. Walifanya kazi kwa heshima, kwa utu. Walikuwa mstari wa mbele. Hakuna mtu mwingine katika ulimwengu huu anayefanya kazi kwa bidii kama walivyofanya.”

Na inaelezwa wapiganaji wengi waliosamehewa, kwa kawaida wanapenda kurudi kwenye jeshi hilo la Wagner kufanya kazi kwa mkataba.

image

Mjumbe UVCCM ataka siasa za hoja badala ya vioja
Muktasari:
Mjumbe wa Baraza Kuu la Umoja wa Vijana wa Chama cha Mapinduzi (UVCCM) Taifa, Victor Makundi amesema Miaka 46 ya CCM iwe kichocheo cha kufanyia kazi changamoto wanazoziona, kuisimamia serikali na kuendesha siasa za hoja badala ya vioja, ikiwa ni pamoja na kuboresha na kuimarisha chama kupitia vikao, mikutano na kuvutia wanachama wapya kwa sera na siasa safi huku akiwakumbusha vijana kuacha kushinda mitandaoni ovyo.
Rombo. Vijana wa Chama cha Mapinduzi, wametakiwa kujipanga kujibu hoja zinazotolewa na wapinzani kwenye mikutano ya hadhara, ikiwa ni pamoja na kuyasema yale mazuri ambayo yanafanywa na serikali, ili kuwawezesha wananchi kuyafahamu na kuendelea kukiamini chama hicho.

Rai hiyo imetolewa na mjumbe wa baraza kuu la Umoja wa Vijana wa Chama cha Mapinduzi (UVCCM) Taifa, Victor Makundi wakati akizungumza na vijana wilayani Rombo, katika maadhimisho ya miaka 46 tangu kuzaliwa kwa CCM.

Makundi amesema Rais Samia Suluhu Hassan ameruhusu mikutano ya hadhara ya vyama vya siasa nchini, hivyo kama vijana wa CCM, wanapaswa kusimama imara na kujipanga kujibu hoja, na asitokee mtu wa kufanya vioja wala kutoa matusi.
Amesema miaka 46 ya CCM ikawe kichocheo cha kufanyia kazi changamoto wanazoziona, kuisimamia serikali na kuendesha siasa za hoja badala ya vioja, ikiwa ni pamoja na kuboresha na kuimarisha chama kupitia vikao, mikutano na kuvutia wanachama wapya kwa sera na siasa safi.

“Kuna neno linasema acha mvua inyeshe tuone panapovuja. Ndugu zangu, Rais ameruhusu mikutano ya hadhara ya vyama vya kisiasa, sisi kama vijana wa CCM tuzidi kusimama imara, tukajibu hoja wala tusifanye vioja na tusitukanane,” amesema Makundi.

Ameongeza kuwa, “Sisi kama vijana wa CCM, tuendelee kuisemea serikali vizuri, yapo mengi yaliyofanyika na yanayoendelea kufanyika, na wananchi hawawezi kufahamu bila sisi kutoka kuwaambia, sasa tukawe mabalozi, tukayaseme yale mazuri yanayofanywa na serikali chini ya CCM.”

Aidha Makundi ametumia pia nafasi hiyo kuwataka vijana kubuni miradi mbalimbali ya kimaendeleo na kuchukua mikopo ya asilimia nne inayotolewa na Halmashauri ya Wilaya kwa vijana na kuendesha miradi hiyo, ili kuweza kujikwamua kiuchumi.

“Ndugu zangu vijana, tuchangamkie fursa zilizopo, serikali imetenga asilimia 10 ya mapato ya ndani ya halmashauri na asilimia 4 ni kwa ajili ya vijana, fedha tumeambiwa zipo, tuache uzembe, tuache kukaa vijiweni, tuache kulalamika na tuache kushinda mitandaoni, sasa tukabuni miradi yetu.”
“Lakini pia niwaase viongozi wa vijana, tuendelee kuupa nguvu umoja wetu, tutunze amani ya nchi, tushirikiane na tuchape kazi kwa bidii”.

Akizungumza mwenyekiti wa UVCCM Wilaya ya Rombo, Evance Mrema amewataka vijana kuwa mstari wa mbele kukemea maovu katika jamii, ikiwemo vitendo vya kikatili, wizi, uporaji na ulevi wa kupindukia.

“Katika maadhimisho haya ya miaka 46 ya kuzaliwa kwa CCM, vijana tunakumbushwa kuwa wazalendo na kutambua tunalo jukumu la kuilinda dola ili iendelee kubaki mikononi mwa CCM”

“Lakini pia kama vijana, tunapaswa kuwa mstari wa mbele kukemea maovu katika jamii, ikiwemo matukio haya ya unyanyasaji na ukatili ambayo yametajwa kuongezeka, pamoja na ulevi wa kupindukia katika jamii”.

Viongozi hao pamoja na viongozi wengine wa UVCCM Wilaya ya Rombo, pia walitembelea shule ya sekondari Mamsera pamoja na Kelamfua, ambapo pamoja na kupanda miti, walizungumza na uongozi wa shule pamoja na wanafunzi, ili kubaini changamoto zilizopo na kuzisemea serikalini, ili ziweze kupatiwa ufumbuzi

image

Ripoti yaonyesha vijana wengi nchini hawana heshima
Muktasari:
Ripoti ya utafiti wa stadi za maisha na maadili kwa vijana imeonyesha asilimia kubwa ya vijana nchini hawana heshima, hawajitambui na hawana ushirikiano kwenye mambo mbalimbali ya kijamii.
Dar es Salaam. Utafiti uliozinduliwa Leo Januari 26, 2023 na Taasisi ya Regional Education Learning Initiative (Reli) kwa kushirikiana na Taasisi ya Uwezo Tanzania umeonyesha kundi kubwa la vijana nchini hawana Maadili na stadi za maisha.

Ripoti hiyo ya ' Assesment of Life Skills and Values in East Africa' iliyofanyika Julai, 2022 imehusisha vijana kuanzia umri wa miaka 13 hadi 17 katika wilaya 34, kaya 11,802 zikihusika na vijana 14,645 walihusishwa kutoka Tanzania Bara.

Utafiti huo umeonyesha kijana mmoja pekee kati ya 10 ana heshima na kujali maadili katika jamii, ambayo ni sawa na asilimia 12.5 ya vijana wote waliohusika katika utafiti huo.
Vilevile, ripoti imeonyesha kuwepo kwa uelewa mdogo wa vijana kujitambua na kutatua tatizo ambapo asilimia 16.8 pekee wana uwezo huo.

Akizungumzia matokeo ya utafiti huo, Mbunge wa Jimbo la Ubungo na mdau wa Elimu, Profesa Kitila Mkumbo amesema uelewa mdogo wa kutatua matatizo na stadi za maisha unasababishwa na hali ya ubora wa elimu.

"Vijana waliohusika kwenye uchunguzi huu wengi wapo shuleni, napata mshituko kuona Wanafunzi Wana uelewa mdogo wa kutatua matatizo na nalihusisha hili na ubora wa elimu yetu," amesema.

"Tukiwekeza hapa kwenye elimu Bora huko mbele kazi itakuwa rahisi kwenye stadi za maisha Kama kujitambua, kutatua matatizo, ushirikiano na heshima," ameongeza.

Upinzani hustawi baada ya minyukano CCM.
Naikumbuka Julai 13, 2011. Mfanyabiashara na kada wa CCM, Rostam Aziz alitokeza kwenye uso wa vyombo vya habari, akitangaza uamuzi uliogubikwa na hasira. Alijiuzulu ubunge na vyeo vyote ndani ya chama, ikiwemo ujumbe wa Halmashauri Kuu ya Taifa (Nec).
Hasira za Rostam hazikuwa mafichoni. Lugha ya mwili jumlisha maneno kichwani ni jawabu la kuchushwa na kilichokuwa kikiendelea ndani ya CCM. Hususan kumhusu yeye. Alihusishwa na vitendo vya ufisadi. Alituhumiwa kwa anguko la CCM hasa majimboni.

Ilikuwa haijafika hata miezi tisa tangu Uchaguzi Mkuu 2010. Matokeo ya uchaguzi uliofanyika Oktoba 30, 2010, yalionesha kuwa urais CCM walipata asilimia 63.8 ya kura zilizopigwa, kutoka asilimia 80.2 mwaka 2005. Wabunge CCM walishinda majimbo 186 (201 kutoka 206 (2005).
Kupungua kwa kura za CCM 2010, kuna athari za kabla na baada. Matokeo ya kuvunjika Baraza la Mawaziri Februari 2008 na falsafa ya “Kujivua Gamba”, iliyoibuliwa na Kamati Kuu CCM. Rostam alikuwa mwathirika wa siasa za 2008, vilevile lawama za baada ya Uchaguzi Mkuu 2010.

Kujivua gamba

Kujivua gamba ni nini? Kwamba kuna wana CCM waliokuwa wakishutumiwa kwa vitendo vya ufisadi. CCM walitaka wajisafishe mithili ya nyoka anavyovua gamba na kurudi ujana. CCM kupitia falsafa ya Kujivua Gamba, walilenga kuwa wapya. Wajitenge na makada wao wenye makandokando.

Rostam alizungumzwa, Waziri Mkuu wa nane, Edward Lowassa, alisemwa. Tena Rostam na Lowassa walikuwa mithili ya mapacha wawili, jinsi walivyozungumzwa. Rostam alipokuwa anatangaza kujiuzulu, alisema alichoshwa na siasa za majitaka. Akajitoa.

Muhtasari kuhusu Rostam na matokeo ya Uchaguzi Mkuu 2010, unatuleta kwenye mjadala kuwa CCM hawajawahi kubomolewa na upinzani, isipokuwa visa vya wao wenyewe ndani kwa ndani. Kasi ya kuwania madaraka huchukua sehemu kubwa.
Mwaka 2005, CCM waliingia kwenye uchaguzi imara kwa sababu hakukuwa na makundi. Kundi lililokuwepo ni moja, likiitwa “Mtandao”. Naam, ndio mtandao uliomuingiza madarakani Rais wa Nne, Jakaya Kikwete.

Wapo wanasiasa walioumizwa na kujeruhiwa kisiasa kutokana na rafu za Mtandao. Waziri Mkuu wa Nne na Katibu Mkuu wa uliokuwa Umoja wa Nchi Huru za Afrika (OAU), Salim Ahmed Salim, alidhalilishwa na kupoteza kabisa hamu ya kufanya siasa.

Salim aliwahi kusema kuwa aligundua kwamba kugombea urais Tanzania ni njia mojawapo ya kujivunjia heshima. Kwa majina aliyopewa, nafasi aliyowekwa, Salim alijiona kupoteza heshima yake aliyoijenga ndani ya taifa na jumuiya za kimataifa.

Siasa za kuchafuana

Siasa za CCM ni za kuchafuana kuliko kuibuka na hoja au kujenga haiba yenye kuvutia wananchi. Bahati mbaya zaidi, imegeuka kuwa mwendo rasmi wa siasa za nchi. Ukitaka kukubalika CCM, unatafuta washindani wako. Unatengeneza kashfa za kuwachafua.

Waziri Mkuu wa Sita, John Malecela na wa Saba, Fredrick Sumaye, kwa pamoja walikuwa na simulizi yenye kuumiza kuelekea Uchaguzi Mkuu 2005. Hata hivyo, bahati kwa CCM ni kuwa Salim, Sumaye na Malecela hawakuwa na makundi imara yenye nongwa.

Laiti Salim angekuwa na kundi, hali isingekuwa salama mwaka 2005. Vivyo hivyo kwa Sumaye na Malecela. Kutoka mwaka 2005 hadi sasa, uanzishaji makundi imekuwa hulka sugu ndani ya CCM. Athari kubwa ilionekana mwaka 2010 na 2015.

Kundi la Mtandao lilianza mwaka 1995. Lilimsumbua aliyekuwa Mwenyekiti wa CCM, Rais wa Pili, Ali Hassan Mwinyi. Likamtikisa mwana CCM aliyekuwa na kadi namba moja, Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere. Kwa Mwalimu aliweza kuwadhibiti.

Mwanzilishi wa Mtandao alikuwa Lowassa. Aliposhirikiana na Spika wa Bunge la Tisa, Samuel Sitta, kumshawishi Rais wa Nne, Jakaya Kikwete, kuwa timu moja kuelekea Uchaguzi Mkuu 1995. Upacha wa Kikwete na Lowassa ukaundwa.

Hata baada ya Lowassa kukatwa jina kwenye Kamati Kuu CCM mwaka 1995, hali haikuwa rahisi kutokana na uwekezaji wa Lowassa. Mwalimu Nyerere alilazimika kutoka mbele ya vyombo vya habari na kutetea uamuzi wa Kamati Kuu.

Kikwete aliposhindwa na Rais wa Tatu, Benjamin Mkapa, kulikuwa na sauti za vijana, walewale waliofanya fujo Lowassa alipokatwa, safari hiyo walimtaka Kikwete asikubali matokeo na atangaze kuhamia upinzani.

Ndio sababu, Kikwete alipokuwa anataka kuongea ndani ya Mkutano Mkuu CCM, aliyekuwa Katibu Mkuu, Lawrence Gama, alikataa kumpa ‘maikrofoni’. Mwalimu Nyerere alipoona hitaji la Kikwete kuongea, akaagiza apewe nafasi.

Kisha, Kikwete akawashangaza wengi alipotangaza kumuunga mkono Mkapa na kuagiza timu yake ijielekeze kwa mgombea aliyeshinda. Ikawa furaha kwa Mwalimu Nyerere, Mwinyi mpaka mgombea mwenyewe, Mkapa.

Kumbe sasa, kama si uimara wa Mwalimu Nyerere na busara za Kikwete kukubali kushindwa, pengine mgawanyiko CCM ungekuwa mkubwa. Vivyo hivyo, endapo Salim, Malecela na Sumaye wangeunda makundi kuelekea Uchaguzi Mkuu 2005, chama kingeenda kwenye uchaguzi kikiwa vipande.

CCM na kikulacho

Historia inaonyesha kuwa methali ya “kikulacho kinguoni mwako”, ndio mtihani mkubwa CCM. Sasa hivi tayari majina yanapenya hadi mitandaoni. Mara Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa hatakiwi, anayetakiwa ni January Makamba.

Mbunge wa zamani wa Arusha Mjini, Godbless Lema, aliandika hivi karibuni kwenye akaunti yake ya Twitter kuwa anazo taarifa za ndani kwamba George Simbachawene ndiye Waziri Mkuu anayefuata baada ya Majaliwa.

Kwa akili ya kawaida unajiuliza, nani anaweza kuvujisha hizi taarifa? Ukimfikiria Rais Samia Suluhu Hassan, utapindisha shingo kukataa. Majaliwa hawezi kujitengenezea nuksi. January na Simbachawene, wanawezaje kuvujisha habari zao kabla ya wakati?

Ukifika hapo, utagundua kwamba haihitaji elimu kubwa ya intelijensia kubaini uwepo wa watu wenye lengo la kumchonganisha Majaliwa na bosi wake, Rais Samia. Majaliwa amtazame Rais Samia kwa jicho la chuki, kuwa hamwamini.

Historia ni mwalimu. Kikwete akiwa Rais na Lowassa Waziri Mkuu, mgogoro wao ulitengenezwa kwa namna iliyowaacha wao wenyewe wakiwa hawaaminiani. Kikwete hakumwamini Lowassa, vivyo hivyo kwa mwenzake. Mwisho, ukaibuka uadui mkubwa wa kisiasa.

Uchonganishi kuhusu Majaliwa na nafasi ya Uwaziri Mkuu, bila shaka, unakusudia kumfanya apoteze imani na wasaidizi wake ambao ni January na Simbachawene. Ajione yupo katikati ya uadui, kwa bosi wake mpaka wasaidizi chini yake.

Lowassa alipokuwa anajiuzulu uwaziri mkuu, alisema kulikuwa na matamanio ambayo yeye aliamua kwenda kuyatimiza. Akasema ni “uwaziri mkuu”. Ilikuwa wakati wa kashfa ya Richmond.

Lowassa alitaka Watanzania wajue kwamba mengi yaliyotendeka ni matamanio ya watu kuona anaachia kiti cha Waziri Mkuu.

Hata sasa, Majaliwa anaweza kuona nafasi yake inatolewa macho sana na kuna watu matamanio yao ni kuona anang’oka. Atamtazama vibaya Rais Samia, hatawaangalia kwa macho ya wema, January na Simbachawene.

Endapo Majaliwa atapata wakati mzuri wa kutafakari, anayetengeneza maneno ndiye mwenye masilahi na cheo chake. Si Samia wala January na Simbachawene. Daima, mchonganishi hujenga fitina akiwa analenga matokeo yenye sura ya mgogoro.

Mnyukano ndani ya CCM

Swali, nani anaweza kuwa na masilahi na uwaziri mkuu wa Majaliwa kwa sasa? Jibu ni moja tu, ni wao wenyewe CCM ndani kwa ndani.

Yupi anakusudia kuona mgawangiko kwenye Serikali ya Samia? Jawabu ni lilelile, CCM wao kwa wao.

Majaliwa aking’oka, atakayepata ni mbunge wa kuchaguliwa kutoka CCM. Hakuna mpinzani mwenye masilahi binafsi na Majaliwa kutenguliwa uwaziri mkuu.

Ukitokea mvurugano wa ndani kwa ndani kwenye Serikali ya Samia, watanufaika wabunge CCM, ikiwa kuna mawaziri wataondolewa, nafasi zitajazwa miongoni mwa wabunge. Na karibu wote ni CCM.

Hivi sasa unaweza kustaajabu January anashambuliwa kuwa ni Waziri wa hovyo. Kisa umeme unakatika. Unajiuliza swali, tangu lini Tanzania ilijihakikishia umeme wa uhakika usiokatika?

Mbona kelele za sasa ni nyingi kuwahi kutokea? Kumbe ni mwangwi ndani ya CCM.

January alisemwa kuwa anahujumu kukamilika kwa mradi wa Bwawa la Kuzalisha Umeme la Julius Nyerere (JNHPP). Kisha tukashuhudia tukio la kuruhusu maji kuingia ndani ili kuanza rasmi kazi ya kufua umeme.

Februari 2022, January alielezea kuwa tatizo la umeme ni miundombinu, hivyo inahitaji muda kuirekebisha. Alieleza changamoto ya nyaya zenye uwezo wa msongo mdogo wa umeme kubeba msongo mkubwa mpaka transfoma yenye uwezo wa kuhudumia nyumba 50 kubebeshwa nyumba zaidi ya 100.

Ukifuatilia jinsi January anavyoshughulikiwa, unapata jibu la mapambano ya wao kwa wao. Atoke January aingie mwingine. Na mara nyingi mapambano ndani ya CCM huwa hayabebi masuala kuhusu wananchi. Ni migogoro ya vyeo.

Mikutano ya hadhara

Kipindi hiki imetolewa ruhusa ya mikutano ya kisiasa. Endapo CCM watapitia kipindi kigumu, yupo mtu anaweza kusingizia ruhusa ya mikutano. Ukweli haupo hivyo.

Vyama na nguvu ya upinzani hutumika kama maficho ya ukweli, maana upinzani haujawahi kuibomoa CCM, bali vita ya ndani.

CCM wangekomesha kwanza makundi na michuano ya urais isiyo na tija. Wamwache Rais, Waziri Mkuu na timu ya mawaziri ifanye kazi. Bunge lifanye kazi ya usimamizi. Vyama vya upinzani vifanye ukosoaji.

Miaka nenda rudi, migogoro ya CCM ndio huwapa agenda wapinzani. Ufisadi lilitoka CCM na kubebwa na wapinzani.

Kama tamaa za urais ndani ya CCM na makundi ya vyeo, vitazidi nguvu za chama na Serikali, upinzani utastawi. CCM itafika 2025 ikiwa vipande.

image